HII NI MAITI YA NANI!!!!!
Nilipokuwa mwanafunzi wa  sekondari, 
niliwahi kushuhudia mwili wa mwanafunzi mwenzetu ukigombewa  na wazazi 
wake. Huyu mwanafunzi mwenzetu alifariki ghafla shuleni na  ikabidi 
wazazi wake wafahamishwe ili waseme maiti isafirishwe kwenda  wapi.
Mama
 alisema, maiti ya mwanaye ibaki hapo alipofia, kwani  atakuja kuichukua
 na kuisafirisha kuipeleka kwao (mama) kwa mazishi.  Baba naye alisema 
hivyo hivyo. Walimu wakaamini kwamba, baba na mama  wanazungumza jambo 
lilelile. Lakini walipowasili pale shuleni, ndipo  walipogundua kwamba, 
hawakuwa wanawasiliana na watu walio pamoja.
Baba alikuwa na dini
 nyingine na mama alikuwa wa dini nyingine na  walishaachana kitambo. 
Tangu walipoachana wazazi hawa, kila mmoja akawa  anamvutia mtoto aingie
 au afuate dini yake. Kwa jinsi tulivyokuwa  tunamfahamu marehemu, 
hakuwa hasa mtu wa dini fulani. Wakati  wa vipindi  vya dini, huyu 
mwenzetu alikuwa anaingia mara kwenye madarasa ya  waislamu, mara 
wakristo na alikuwa anaingia kwenye madhehebu mbalimbali.
Basi, 
wazazi hawa walikuwa kila mmoja akitaka kuchukua mwili wa  marehemu. 
Kila mmoja alikuwa akitoa maelezo ni kwa nini yeye ndiye  anayestahili 
kumzika mtoto kwa dini yake. Malumbano haya yalikuwa  makubwa mpaka 
vyombo vya dola vikahusishwa. Nakumbuka alikuja afisa  mmoja wa 
upelelezi kwenye malumbano hayo. Katika kujaribu kutafuta  muafaka, 
afisa huyu alizungumza kama vile kwa kuhutubia akisema: " Inasikitisha 
kwamba, kijana wetu mpendwa, anaingizwa kwenye choyo na  ubabe wa 
kuoneshana nani zaidi, katika hali hii ambapo hawezi kujitetea.  
Naamini, huyu marehemu kwa sasa anawachukia wazazi wake wote, kwani  
anajua wazi hakuna anayempenda hata mmoja, bali wanatumia kifo  chake  
kama uwanja tu wa mapambano ya kujitosha kwao.
Naamini, hivi sasa
  marehemu angeombwa kuchagua rafiki na ndugu wa kweli, angechagua  
wanafunzi wenzake na walimu wa dini. Hii inatokana na ukweli kwamba,  
hawa hawakutaka kumpangia aabudu au kuifuata imani gani ya dini.  
Tunaambiwa aliingia kwa waislamu, na aliingia kwa wakristo pia,  
hakuzuiwa au kusemewa, alikuwa huru.
Kuwa na dini ni kuwa na 
uhuru.  Kuwa na dini ni kuwapa wengine uhuru wa kuwa wao. Kuwa na dini 
siyo  kutumia tatizo la mwingine kujifaharisha, kuonesha ubabe na 
urijali  ulionao. Hiyo ni kibri ambayo kwa mtu aliyepoteza mwili kama 
huyu kijana  wetu anaiona na kuijua vizuri, haipendi hali hii..."
Hotuba
 hiyo  ilisaidia sana, kwani hatimaye ndugu wa upande wa mama na wale wa
 upande  wa baba walikaa chini wakiwa na adabu mpya na kujadili. 
Hatimaye  walikubaliana kijana azikwe kwa dini ya mama yake.
Miaka
 30 baadaye,  nakutana tena na watu wanaogombea  maiti, watu wanaoamini 
kwamba mzoga  wa binadamu una maana yoyote. Sijawahi kuona mtu akitoa 
shati au gauni  kwenye mfuko wa nailoni na kuvaa mfuko huo badala ya 
kuvaa shati au  gauni, nimesema sijawahi kuona, huko ni kujidanganya. 
Nimekuwa nikiona  sana jambo hilo, ambapo ni pale watu wanapogombea 
mwili.
Inaonesha  wazi kwamba, binadamu bado ni mjinga sana juu 
ya maisha yake. Mwili,  mwili ni nini, na hadi wapi? Kama mwili ungekuwa
 na maana sana, baada ya  mtu kufariki usingekimbizwa mochuari, 
usingepakwa asali au usingechomwa  sindano ili usiharibike na kuleta 
usumbufu wa harufu na maradhi. Mwili  siyo mimi wala wewe. Mwili 
haujawahi kuwa mwenye mwili na hautakuja  kuwa. Mwili ni kama tochi tu, 
ambayo umeiazima ili iweze kukusaidia  kufika kijiji cha pili, kutokana 
na giza na njia ya uchochoro ambayo  unatakiwa kuipita ili kufika kijiji
 hicho cha pili. Mwili ni kifaa na  siyo wewe, bali wewe unakitumia 
kifaa hicho Binadamu anajibainisha  kwenye maisha haya ya hapa duniani 
kupitia mwili wake, lakini yeye siyo  mwili.
Mwili ni ubainisho, 
ni chombo cha kutumika kwa kusudi la kidunia  tu. Baada ya muda mwili 
hukoma kuwepo, hujimaliza wenyewe au kumalizwa,  ili binadamu amudu 
kuingia hatua nyingine ya maisha ambayo haitumii au  haihitaji mwili. 
Tangu ulipozaliwa umeoneshwa na kufundishwa kwamba,  wewe ni mwili kwa 
njia zote. Akili yako imeshika kutu kwa kuamini  kwamba, mwili ni wewe 
na wewe ni mwili. Huna uwezo tena wa kuuona  ukweli, kwa sababu vipimo 
vyako vyote kuhusu maisha vinaishia kwenye  akili, ambayo nayo pia 
haikuhusu, siyo yako, umepachikwa tu.
Kwa  ujinga huu wa kutojua 
mwili ni nini na sisi ni nani, ndipo ambapo  tunaingia kwenye ujinga wa 
kuendeshwa na miili yetu, hisia zetu na  akili. Kila mmoja anaamini 
kwamba, mwili wake ukipotea, ukishindwa  kutumika, yaani akifa, basi huo
 ndiyo mwisho wake. Kama hiyo ni kweli,  ina maana binadamu hana maana 
kabisa, ni upuuzi usiofaa kuelezewa!
Yaani  binadamu amekuwepo 
ili awepo kwa mwezi mmoja, miaka kumi, hamsini,  sabini, tisini, au mia 
tu. Halafu baada ya hapo basi. Huu ni uongo  mkubwa sana, unaoweza 
kukubaliwa na akili makapi ya kulishwa tu!  Anayetafakari zaidi kidogo, 
atabaini kwamba, mwili ni mwili tu, ni kasha  tu.
Ni kasha ambalo
 muda wake wa kutumika ukiisha mtumiaji au  [wewe] analiacha kwa sababu 
haliwezi kukidhi kile anachokihitaji hapa  duniani. Mtumiaji anachukua 
kingine ambacho kinakidhi wakati huo [baada  ya kifo]. Kwa hiyo, 
binadamu hafi bali mwili ndiyo unaofikia ukomo wa  muda wake wa matumizi
 kwa sababu mbalimbali. Anapokufa John au Hamisi,  haina tofauti. 
Anapokufa mkulima hohehahe au tajiri kuliko wote duniani,  pia haina 
tofauti. Wote wanapita kwenye hatua muhimu ya mabadiliko,  ambapo 
wanaacha matumizi ya kifaa kilicho kuwa ndicho pekee kinachoweza  
kuwabainisha na wengine hapa duniani na kuchukua kingine ambacho  
hakiwezi kuwabainisha tena na wale wenye miili bado.
Anapokufa 
John au  Hamisi, haijalishi kama amezikwa kwa jeneza la dhahabu na 
mizinga 100 au  kwa masululu butu na kaniki. Kuzikwa ni utaratibu wa 
kimazoea wa  kuhifadhi mwili ambao sasa ni mzoga tu, ili usisumbue watu 
wengine kwa  harufu na maradhi. Kuzika haina maana kwamba, kunambadili 
aliyekuwa  akitumia mwili huo [marehemu], la hasha. Kama unadhani kwamba
 Mungu  anahesabu umezikwa na dini gani, umezikwa na shehe au padri 
gani, ndiyo  afanye uamuzi wa kukupokea mbinguni au hapana, ujue 
unahitaji msaada wa  haraka, kama siyo kupelekwa milembe. Ujue hujui 
chochote ingawa umekuwa  ukujidanganya kwamba unajua.
Mungu wa 
kweli hahangaiki na mzoga,  bali sisi kwa ufinyu wetu ndiyo tunaodhani 
kwamba, mizoga au[maiti] hii  ina maana. Mara nyingi nimekuwa 
nikiwaambia jamaa zangu, ‘nikifa,  mtaangalia ni mazingira gani ni 
rahisi kwenu kuutupa au kuuhifadhi mwili  wangu. Kwa nini? Kwa sababu, 
kama sikuwa karibu na Mungu wakati nikiwa  na mwili, huo, ukaribu 
utaletwa leo wakati nimeupoteza mwili huo kwa  sababu tu, mwili wangu 
umezikwa kwa dini ya babu yangu? Ukosefu wa  ufahamu wa kiwango kikubwa 
sana. Kama nilikuwa karibu na Mungu wakati wa  uhai wangu, basi hata 
nikitupwa ****** baada ya kufa, ukaribu huo  hautakufa. Mungu hayatazami
 mambo kama Abdallah Juma au John Maiko!  Kwani kuzika hasa ni kitu 
gani?
Hatuziki watu ili waende mbinguni. Kama  ni hivyo, 
wanaoliwa na wanyama, kuungua na kuteketea kabisa, wao  Mbinguni 
hawatafika? Kama hawatafika, watahukumiwa vipi siku ya mwisho?  Mwili 
hautakiwi Mbinguni, hauna kazi huko, kwani huko siyo makazi ya  miili. 
Mwili unafaa tu duniani Kuna zile jamii ambapo mtu akifa mwili  wake 
huchomwa moto na kuteketezwa kabisa Unadhani hizi jamii hazimjui  Mungu 
kama wewe unavyomjua? Zinamjua, tena pengine vizuri zaidi yako.  Lakini,
 zimeng’amua kwamba, mwili ni kasha tu, likishindwa kufanya kazi,  ni 
sawa na taka nyingine, hutupwa dampo na kuteketezwa kwa moto.  Mtu  
akishauacha mwili wake [kufa] hana tena uhusiano na mwili huo. Mtu huyo 
 anakuwa ameingia kwenye awamu nyingine ya maisha ambayo haihitaji mwili
  na ambayo haihitaji kujua huo mwili umezikwa na nani na wapi. Ni akili
  isiosogea ndiyo ambayo inashindwa kufanya mikokotoo midogo kama hii.
Ukiona
 watu wanagombea maiti, jua kwamba, hata kama wamevaa masuti na  
kubandika digrii zao kwenye kila ukuta, ni watoto wadogo kiufahamu.  
Ukiona mtu pia anaacha wosia mrefu wa namna anavyotaka akifa azikwe,  
naye huyo ni mpujufu tu wa ufahamu. Kwa nini? Unagombea kuuzika mwili wa
  fulani ili upate kitu gani, ili huyo marehemu naye apate nini? Hata  
usipouzika, kumbuka kwamba, ameshakufa na ukiuzika, ameshakufa pia.  
Haifanyi tofauti yoyote kwa kweli. Kama nilivyosema awali, huuziki mwili
  ili uende Mbinguni kwa sababu mbingu haiko ardhini. Unaufukia ili  
usisumbue kwa harufu.
Ukienda kwenye nchi zenye vita hasa vya  
wenyewe kwa wenyewe, utagundua kirahisi kwamba, maiti hana maana, maiti 
 ni msumbufu kwa kunuka na kusambaza magonjwa. Tunazika kwa sababu tuna 
 nafasi ya kuhifadhi mwili kwa heshima na taratibu ambazo zinaonesha  
kujali mwili wa mwenzetu ambao ulitumika kufanya mema au maovu. Kwenye  
kizuizi na misukosuko au vita, hakuna anayeweza kukumbuka, siyo kuzika  
bali hata kufukia maiti. Kila mmoja anafikiria kuendelea kubaki na mwili
  wake kwanza. Aliyepoteza wake, basi hakuna anayemjali, kwani haina  
maana kabisa kumjali.                      Hata aina nyingine za mazishi
  zinaonesha tu ujinga na utoto wa binadamu.
Mazishi ya          
                           kifahari yenye kuhusisha majeneza ya dhahabu 
na  vyakula na vinywaji vya bei mbaya. Ni ujinga uliopindukia kwa 
sababu,  inawezekana kabisa marehemu au wanaotoa fedha hizo hawajawahi 
kumsaidia  aliye hai hata kwa chupi ya mguu. Sasa kusaidia huo mzoga kwa
 mapambo  inaongeza kitu gani? Nimesema unapoona mtu anaacha wosia ili 
azikwe  vipi, wosia ambao wakati mwingine ni kero tupu, ujue huyo naye 
ni mtoto  wa miaka sita, bila kujali anamiliki au amesoma hadi kiwago 
gani. Ni  utoto kwa sababu, unapoacha mwili, siyo kazi yako kusema huo 
mwili  ufanyiwe kitu gani. Waliobaki, wanaweza kuamua kuuchoma mishikaki
 [kama  wanakula watu], wanaweza kuukausha na kuuweka kwa maonesho, 
wanaweza  kuufukia kwenye kijishimo cha futi tano na ukafukuliwa na fisi
 usiku, na  wanaweza kuuzika kwa matarumbeta na sanduku la dhahamu. Ni 
hiari yao.  Ukishauacha mwili huna mamlaka nao tena.
Ni wale 
waliobaki ndiyo  wanaolimbuka nao tu. Nimekuwa nikitazama hii tabia ya 
kugombea maiti kwa  jicho lenye mashaka na ufahamu wa binadamu, hofu 
zake na ufisadi wa  nafsi alionao. Mtu amekufa, wewe unasema nataka 
nimzike mimi, sawa.  Kwani mbona huendi hospitalini ukaulizia maiti 
ambazo hazina ndugu na  kuzichukua ili ukazizike? Wewe si unapenda 
kuzika na unaamini kumzika  mtu kwa dini yako ni jambo kubwa na la maana
 sana? Pia hospitalini,  utapewa maiti nyingi zisizo na ndugu. 
Ukishazipata zibadili majina na  kuziingiza kwenye dini yako kwa mujibu 
wa utaratibu wa dini yako. Halafu  zika! Hiyo huitaki kwa sababu haina 
maslahi, haina kuonesha ubabe ambao  umefundishwa na wazazi, na jamii na
 pengine hata na dini yako hiyohiyo.  Kugombea maiti ni kujiogopa.
Kugombea
 maiti ni kujitafuta kimakosa.  Kugombea maiti ni kutojua dini. Kugombea
 maiti ni kudhani mtu anaweza  kuwa na uhuru wa kuwa mtu mwingine. 
Kugombea maiti ni kufikiri wewe ni  mwili, Kugombea maiti ni njaa ya 
mali au haja ya kupanda kithamani. Kwa  ujumla ni ubabe wa kimtaa zaidi.
 Mara nyingi imeshatokea, anapookotwa  maiti na watu wakaanza kuulizana,
 jamani maiti hii ni ya nani? Ujue  maiti hiyo itazikwa na serikali. 
Hakuna mtu au kundi la kidini la eneo  hilo ambalo litajitokeza 
kuichukua na kuizika maiti hiyo kwa imani yake.  Hilo haliwezekani kwa 
sababu halina utamu.
Halina kubishana, halina  kulumbana, halina 
ujuaji na ubabe. Anasubiriwa mtoto mwenye mzazi  walioachana na walio na
 dini tofauti. Huyu akifa, hasira na visasi vyote  vya nyuma vinaishia 
kwenye mwili wake. Atasubiliwa yule ambaye  alishakuwa kwenye dini yetu 
akatoka, huyo akifa
tuna sababu ya  kugombea maiti. Kama nilivyosema,
 hapo kuna malumbano  na ujuaji na  kuoneshana. Halafu bado mnajiita 
mnatumikia dini, zipi? Ni ujinga tu.