Recent Posts

PropellerAds

Thursday, March 31, 2016

MAGAZETI YA LEO TZ,APRIL MOSI

Wafadhili wasitisha ufadhili kwa bajeti ya Tanzania

Mataifa 10 ya Magharibi yamesema hayataendelea na
ufadhili wao kwa bajeti ya serikali ya Tanzania.
Baadhi ya nchi hizo ni Sweden na Ireland. Nchi hizo
zinaendelea na msimamo huo ikiwa ni siku chache
baada ya shirika la utoaji misaada la serikali ya
marekani (MCC) kuondoa msaada wake wa dola 472
za ufadhili wa miradi ya maendeleo kwa Tanzania.
Bodi ya MCC ilisema hatua yake ilitokana na mzozo
kuhusu uchaguzi wa kisiwa cha Zanzibar na utekelezwaji
wa Sheria ya Uhalifu wa Mtandao.
Mataifa yaliyositisha ufadhili wao kwa bajeti ya Tanzania
hata hivyo hayajaeleza sababu ya kufanya hivyo.
Ubalozi wa Sweden umethibitisha kwamba taifa hilo
limesitisha ufadhili wake kwa bajeti ya Tanzania, lakini
ukasisitiza kwamba hatua hiyo haihusiani na yaliyojiri
katika uchaguzi wa visiwa vya Zanzibar.
Tanzania yasikitika kunyimwa pesa za MCC
Uchaguzi wa Zanzibar waikosesha hela Tanzania
"Mwaka uliopita, Sweden ilikuwa moja ya nchi
zilizositisha ufadhili wake kwa bajeti ya Tanzania
kutokana na tuhuma za ufisadi kuhusiana na sekta ya
kawi [na mkataba wetu na serikali ulifika kikomo
mwaka jana],” ubalozi huo umeambia BBC.
“ Sweden inafurahishwa na juhudi za serikali kukabiliana
na ufisadi na iko tayari kuanzisha majadiliano na
serikali ya Tanzania na wafadhili wengine kuhusu
mikakati ya kufadhili bajeti ya Tanzania siku zijazo.”
Ubalozi wa Ireland pia umethibitisha kwamba ni kweli
taifa hilo halifadhili tena bajeti ya Tanzania.
Ufadhili wake wa mwisho ulitolewa mwaka wa kifedha
wa 14/15, malipo ambayo yalifanyika Juni 2015 na
kwa sasa hakuna malipo yaliyoratibiwa ya mwaka wa
kifedha wa 15/16.
"Mpango ulimalizika Juni 2015 na hakuna mipango
mingine ya kutoa ufadhili kwa bajeti (ya Tanzania),”
ubalozi wa nchi hiyo umesema.
Karibu theluthi moja ya bajeti ya Tanzania ilitegemea
msaada mwaka uliopita, kwa hivyo hatua ya nchi hizo
ni pigo kwa mipango ya maendeleo ya serikali mpya.

Aliyewakinga wakristo kutoka kwa al shabab atuzwa

Marehemu mwalimu aliyepigwa risasi akiwakinga wakristo
wasiuawe na magaidi wa Al Shabab ametuzwa medali
ya juu zaidi na rais wa Kenya Uhuru Kenyatta
Rais Kenyatta alipokuwa akihutubia taifa alisema kuwa
wale wakenya wachache wanaoonesha ujasiri wa
kukabiliana dhidi ya al shabab watatuzwa.
Rais Kenyatta alihutubia taifa
Na hivyo akasema kuwa Mwalimu Farah ametuzwa
heshima ya juu zaidi nchini Kenya ya' Order Of The
Grand Warrior', kwa ujasiri wake dhidi ya magaidi.
Marehemu Salah Farah alikuwa katika basi lililokuwa
likiwasafirisha abiria kutoka mji mkuu wa Nairobi
kuelekea Mandera walipotekwa na wapiganaji wa Al
shabab.
Punde wapiganaji hao wakaanza kuwagawanya waislamu
na wale wasio waislamu.
Al Shabaab: Wanawake waislamu waliwafunika Hijab
wakristo
Waislamu waokoa wakristo waliotekwa na al Shabab
Hapo ndipo Mwalimu Farah na abiria wengine waislamu
waliponga'amua nia ya wapiganaji hao ilikuwa ni kuua
wakristu , waliibua mbinu ya kuwakinga abiria wakristo
miongoni mwao ilikuokoa maisha yao.
Farah na wenzake wawili walijeruhiwa vibaya baada ya
kukataa kugawanywa kwa makundi.
Kwa bahati mbata Mwalimu Farah alifariki mwezi
Januari baada ya kuuguza majeraha ya risasi kwa
takriban mwezi mmoja.
Tukio hilo la kijasiri lilichochea umoja miongoni mwa
wakenya ambao wameshambuliwa mara kadhaa na
magaidi wa Al Shabab.
Hiyo ilikuwa ni mara ya pili basi la kampuni hiyo ya
Makkah kutekwa.
Mwezi Novemba mwaka uliopita wapiganaji wa Al
Shabaab waliteka basi moja na kuwaua abiria 28
ambao hawakuwa waislamu.
Kundi hilo liligonga vichwa vya habari mwezi Aprili
mwaka uliopita lilipowaua wanafunzi wakristo 148 katika
chuo kikuu cha Garissa.

Mwana wa Besigye awania urais Oxford

Mwana wa kiongozi wa upinzani nchini Uganda Kizza
Besigye ni miongoni mwa wanafunzi waliojitokeza
kuwania urais katika chama cha mijadala chuo cha
Oxford.
Anselm Besigye ametengeneza video fupi ya kuwaomba
wanafunzi wenzake wampigie kura.
Anasimulia mambo ambayo amefanyia chama hicho na
uzoefu wake katika mijadala.
Mwisho wa video mamake Anselam Winnie Besigye,
anaonekana na kusema “huna budi kushinda uchaguzi
huu, nimekusaidia sana!”.
Babake Anslem, Dkt Kizza Besigye, amewania urais
mara nne dhidi ya kiongozi wa muda mrefu wa Uganda
Yoweri Museveni bila mafanikio.
Anazuiliwa kwake nyumbani na maafisa wa usalama
tangu kufanyika kwa uchaguzi mkuu tarehe 20 Februari.

Waziri wa Rwanda afia gerezani Burundi

Waziri wa zamani wa Rwanda Jacques Bihozagara
amefariki katika gereza moja nchini Burundi miezi minne
baada ya kukamatwa kwa tuhuma za kufanya ujasusi.
Rwanda imesema marehemu Jacques alikuwa ameshikiliwa
kinyume cha sheria.
Balozi wa Rwanda nchini Ubelgiji ameandika na kusema
kifo cha Jacques ni "mauaji".
Wafungwa katika gereza alipokuwa ameshikiliwa
wanasema alionekana akiwa katika hali nzuri na kwamba
alifariki dakika chache baada ya kuchukuliwa kutoka
gereza kupelekwa hospitali baada ya kuugua.
Umoja wa Mataifa umekuwa ukiishutumu Rwanda kwa
kujaribu kuipindua serikali ya Rais wa Burundi Pierre
Nkurunziza, madai ambayo Rwanda imekuwa
ikiyakanusha.

Wafadhili wasitisha misaada kwa Tanzania

Kundi la watoa misaada 10 kutoka nchi za magharibi
wametangaza kusitisha ufadhili wao kwa bajeti ya
serikali ya Tanzania.
Hii inafuatia uamuzi wa shirika la utoaji misaada la
serikali ya marekani kuondoa msaada wa dola 472 wa
kufadhili miradi ya maendeleo kutokana na jinsi uchaguzi
wa kisiwa cha Zanzibar ulivyoendeshwa.
Karibu theluthi moja ya bajeti ya Tanzania ilitegemea
msaada mwaka uliopita, kwa hivyo hatua hizo za hivi
punde ni pigo kwa mipango ya maendeleo ya serikali
mpya.

Daraja laporomoka na kuwaua 10 India

Takriban watu 10 wameuawa na wengine kadhaa
kujeruhiwa baada ya daraja moja la juu lililokuwa
likijengwa kuporomoka kwenye mji wa mashariki mwa
India wa Kolkata
Ripoti zingine zinasema kuwa karibu watu 150 huenda
wamekwama chini ya vifusi vya daraja hilo lililo eneo
lenye shughuli nyingi.
Miradi ya ujenzi nchini India mara nyingi imekumbwa
na matatizo ya kiusalama na huporomoka mara kwa
mara.
Wataalamu wanasema kuwa, huwa kuna ukosefu wa
ukaguzi wa miradi na matumizi ya vifaa duni katika
ujenzi.

Chama chatisha kumuondoa Zuma madarakani

Chama cha Democtratic Alliance nchini Afrika Kusini
kumeanzisha kampeni ya kumuondoa rais Jacob Zuma
madarakani baada ya mahakama ya kikatiba kutoa
uamuzi kuwa alikiuka katiba.
Mahakama ilipata kuwa bwana Zuma alikataa kutii agizo
kutoka kwa ofisi ya mwendesha mashtaka mkuu mwaka
2014 la kamtaka alipe pesa zilizotumika kuifanyia
ukarabati nyumba yake ya kibinafsi.
Vyama viwili vya upinzani viliwasilisha kesi hiyo
mahakamani ili kumlazimu rais Jacob Zuma kuzingatia
matokeo ya uchunguzi yaliofanywa na mkaguzi wa hesabu
za serikali, kwamba alihusika na mabadiliko yaliofanyiwa
nyumba yake ya Nkandla.
Mamilioni ya madola yalitumika katika kile kilitajwa na
serikali kuwa uimarishaji wa usalama. Marekebisho hayo
yalishirikisha ukumbi,kidimbwi cha kuogelea na zizi la
ngombe

Trump ayumbayumba kuhusu utoaji mimba

Mgombea urais wa chama cha Republican nchini
Marekani Donald Trump amebadili msimamo wake muda
mfupi baada ya kusema wanawake wanaotoa mimba
wanafaa kuadhibiwa, utoaji mimba ukiharamishwa.
Alikuwa ametoa tamko lake katika hafla iliyopeperushwa
moja kwa moja na kituo cha runinga cha MSNBC.
Hatua hiyo ilimfanya kushutumiwa vikali.
Lakini muda muda mfupi baadaye, alibadili msimamo
wake na kusema ni wahudumu wa afya wanaosaidia
wanawake kutoa mimba pekee wanaofaa kuadhibiwa.
Lakini hata baada ya kusema hivyo, alijitetea na
kuongeza kuwa: “Msimamo wangu haujabadilika.”
Mgombea huyo anayeongoza katika chama cha
Republican anaunga mkono kupigwa marufuku kwa utoaji
mimba, lakini kwa kutegemea hali.
Utoaji mimba umekuwa halali nchini Marekani tangu
1973 kufuatia uamuzi wa kihistoria wa Mahakama ya
Juu nchini humo.
Trump aahidi kuvunja mkataba wa nyuklia
Trump akemewa kwa matamshi kuhusu Waislamu
Mambo 20 makuu anayoamini Donald Trump
Ni kupitia Mahakama Kuu pekee au marekebisho ya
katiba ambapo uamuzi huo katika kesi ya Roe v Wade
unaweza kubatilishwa na uavyaji mimba kuharamishwa.
Bw Trump, ambaye wakati mmoja alikuwa mfuasi wa
chama cha Democratic, ameshutumiwa awali kwa kutetea
haki za wanawake kutoa mimba.
Msimamo rasmi wa chama cha Republican ni kwamba
utoaji mimba unafaa kuwa haramu.
Wanasiasawahafidhina na wanaharakati wanaochukulia
utoaji mimba kuwa sawa na mauaji, hata hivyo, mara
nyingi hukwepa kuwekea lawama wanawake wanaotoa
mimba na badala yake kuwalaumu wanaowasaidia
wanawake kutoa mimba.
Lengo kuu la hili huwa kuvutia wananchi ambao kimsingi
hawawezi wakafurahia kuwaona wanawake wengi
walioshika mimba kimakosa wakifungwa jela kwa kutoa
mimba.
Viongozi wa chama cha Republican wameeleza wasiwasi
wao kuhusu kuidhinishwa kwa Bw Trump kuwa mgombea
wa chama hicho katika uchaguzi mkuu Novemba, hasa
kwa sababu kura za maoni zinaonesha hapendwi sana
na wapiga kura wa kike.
Bw Trump ameshutumiwa kwa kuwadhalilisha wanawake
wakiwemo aliyekuwa mgombea urais Carly Fiorina na
mtangazaji wa runinga Megyn Kelly.
Meneja wake, Corey Lewandowski, alikamatwa Jumanne
akituhumiwa kumshambulia mwanahabari wa kike.
Bw Trump amemtetea Bw Lewandowski akisema
hakutenda kosa lolote.

Wednesday, March 30, 2016

HOTUBA YA TRUMP YATUMIKA KATIKA FILAMU

Wazalishaji wa filamu moja nchini Mexico kuhusu
wahamiaji wanaojaribu kuingia nchini Marekani wametoa
kipande kidogo cha filamu hiyo ambacho kinatumia
hotuba ya bwana Donald Trump kupitisha ujumbe wa
filamu hiyo kwamba maneno ni hatari kama risasi.
Sauti iliowekwa katika filamu hiyo ya Kihispania,
Desierto ,inemuonyesha bwana Trump akiitaka Mexico
kusitisha kuwaingiza Marekani walanguzi wa dawa za
kulevya pamoja na walanguzi wa binaadamu haraka
iwezekanavyo.
Kipande hicho cha filamu kinaisha na mlinzi mmoja
akiwawinda wahamiaji jangwani.Filamu hiyo inaigizwa na
Garcia Gael Bernal na inaelekezwa na Jonas Cuaron
,mwanawe mwelekezi aliyeshinda tuzo za Oscar Alfonso
Cuaron

MAGAZETI YA LEO MARCH 31

Ajali ya ndege yawaua watu 7 Canada

Watu saba wamefariki baada ya ndege moja ya kibinafsi
kuanguka katika kisiwa cha mashariki ya pwani ya
Quebec.
Mamlaka imesema kuwa ndege hiyo ilianguka ilipokuwa
ikikaribia uwanja wa ndege wa Madeleine huku kukiwa
na upepo mkali pamoja na barafu.
Jean Lapierre,aliyekuwa waziri wa uchukuzi nchini
Canada pamoja na watu wa familia yake walikuwa
miongoni mwa waathiriwa.
Bwana Lapierre mwenye umri wa miaka 59,alifanya kazi
kama mchanganuzi wa CTV pamoja na vyombo vyengine
vya habari.
Mojawapo ya vituo hivyo TVA kilisema mkewe Lapierre
,nduguze wawili na dadaake mmoja walifariki katika
ajali hiyo.

Marekani yalalamikia UN kuhusu Iran

Marekani na washirika wake kutoka Ulaya
wameulalamikia Umoja wa Mataifa kuhusu hatua ya Iran
ya kufanyia majaribio makombora ya masafa marefu.
Mataifa hayo yamesema majaribio hayo yanakiuka azimio
la Umoja wa Mataifa.
Azimio hilo ambalo liliidhinisha mkataba wa nyuklia
baina ya UN na Iran liliitaka Iran kutofanyia majaribio
makombora ya masafa marefu yenye uwezo wa kubeba
silaha za nyuklia.
Trump aahidi kuvunja mkataba wa nyuklia
Iran yaanza kutekeleza mkataba wa nyuklia
Kwenye barua, iliyopatikana na Reuters, maafisa wa
Marekani, Uingereza, Ufaransa na Ujerumani wameeleza
wasiwasi wao kuhusiana na madai ya Iran kwamba
makombora hayo yameungwa mahususi kuwa tishio kwa
Israel.
Mataifa hayo manne yameliomba Baraza la Usalama la
Umoja wa Mataifa kujadili hatua zinazofaa kuchukuliwa.
Hata hivyo, hayakusema waziwazi kwamba majaribio
hayo ya makombora yanakiuka azimio la Umoja wa
Mataifa kuhusu Iran.
Makombora hayo yalikuwa yameandikwa kauli mbiu:
“Israel sharti iangamizwe”, ikiwa imeandikwa kwa
Kiyahudi.

Monday, March 28, 2016

MAGAZETI YA LEO TZ,MARCH 29