Recent Posts

PropellerAds

Friday, April 27, 2018

Kwa Nini Uonyeshe Shukrani?

Asante sana kwa kuwa chanzo cha kitia-moyo kwangu. Hata ingawa huenda usijue, utu wako wenye kujenga na maneno yenye fadhili yamenisaidia sana.”—Jennifer.
JE, UMEWAHI kupokea ujumbe wa shukrani bila kutarajia? Ikiwa ndivyo, bila shaka ujumbe huo ulikuchangamsha moyo. Kwa kweli, ni jambo la kawaida kutaka kuhisi unathaminiwa.—Mathayo 25:19-23.
Wonyesho wa shukrani unaimarisha uhusiano kati ya anayetoa na anayepokea. Zaidi ya hilo, mtu anayeonyesha uthamini anafuata hatua za Yesu Kristo ambaye sikuzote alitambua matendo mema ya wengine.—Marko 14:3-9; Luka 21:1-4.
Kwa kusikitisha, watu wengi hawaonyeshi shukrani, iwe ni kwa maneno au kwa ujumbe ulioandikwa. Biblia ilionya kwamba katika “siku za mwisho,” watu wangekuwa “wasio na shukrani.” (2 Timotheo 3:1, 2) Tusipokuwa waangalifu, ukosefu wa shukrani ulioenea siku hizi unaweza kuathiri hisia zozote za uthamini ambazo huenda tukawa nazo.
Ni hatua gani ambazo wazazi wanaweza kuchukua ili kufundisha watoto wao jinsi ya kuwa na uthamini? Tunapaswa kumwonyesha nani shukrani? Na kwa nini tuwe na uthamini hata ingawa watu wanaotuzunguka hawana shukrani?
Katika Familia
Wazazi wanafanya kazi ngumu ili kuwaandalia watoto mahitaji yao. Hata hivyo, wakati mwingine huenda wazazi wakahisi kwamba jitihada zao hazithaminiwi. Wanaweza kufanya nini ili kurekebisha hali hiyo? Kuna mambo matatu yanayohitajika.
(1) Mfano. Kama ilivyo na mambo mengine unayomfundisha mtoto, mfano unakuwa na matokeo mazuri. Ikizungumza kuhusu mama mwenye bidii katika Israeli la kale, Biblia inasema: “Watoto wake huamka na kumshukuru.” Watoto hao walijifunzia wapi kuonyesha shukrani? Sehemu inayobaki ya mstari huo inatupa jibu. Inasema: “Mumewe huimba sifa zake.” (Methali 31:28BHN) Wazazi wanaoonyeshana uthamini wanaonyesha watoto wao kwamba mtu anapoonyeshwa uthamini anafurahi, uhusiano katika familia unakuwa bora, na ni ishara ya ukomavu.
Baba mmoja anayeitwa Stephen anasema, “Nimejaribu kuwawekea watoto wangu mfano mzuri kwa kumshukuru mke wangu kwa ajili ya chakula cha jioni.” Matokeo yamekuwa nini? “Binti zangu wawili wametambua jambo hilo, na hilo limewasaidia kutambua umuhimu wa kuonyesha shukrani,” anasema Stephen. Ikiwa umeoa, je, wewe unamshukuru kwa kawaida mwenzi wako kwa ajili ya kazi za kawaida ambazo huenda zisitambuliwe? Je, unawashukuru watoto wako, hata wanapofanya mambo ambayo wanatarajiwa kufanya?
(2) Kuwazoeza watoto. Hisia za kuonyesha shukrani ni kama maua. Zinahitaji kupaliliwa ili ziwe na matokeo bora. Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao jinsi gani wakuze na kuonyesha uthamini? Mfalme Sulemani mwenye hekima alionyesha jambo moja muhimu alipoandika hivi: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.”—Methali 15:28.
Wazazi, je, mnaweza kuwazoeza watoto wenu wafikirie jitihada na ukarimu unaohusika mtu anapotoa zawadi? Kutafakari kwa njia hiyo kunamsaidia mtu akuze uthamini. Maria ambaye amewalea watoto watatu anasema hivi: “Wakati unahusika kuketi na watoto wako na kuwaeleza kinachohusika mtu anapowapa zawadi. Unahitaji kuwaambia kwamba mtu aliwafikiria kibinafsi na akataka kuwaonyesha anawajali kwa kadiri gani. Lakini jitihada hizo zinakuwa na matokeo mazuri.” Mazungumzo kama hayo yanawasaidia watoto wajifunze si tu kile wanachopaswa kusema wanaposhukuru lakini pia kwa nini wanapaswa kushukuru.
Wazazi wenye hekima wanawasaidia watoto wao waepuke kufikiria kwamba ni haki yao kupata vitu vyote vizuri.* Onyo hili linalopatikana katika Methali 29:21 kuhusu kushughulika na watumishi linaweza kutumika hata kuhusiana na watoto: “Mtu akimbembeleza mtumishi wake tangu ujanani, katika maisha yake ya baadaye hata atakuwa mtu asiye na shukrani.”
Watoto wanaweza kusaidiwa jinsi gani kuonyesha uthamini? Linda, mama mwenye watoto watatu, anasema, “Mimi na mume wangu tuliwatia moyo watoto wetu wachangie katika ujumbe wa shukrani kwa kuchora picha au kwa kuandika majina yao katika kadi.” Ni kweli, picha yenyewe inaweza kuwa sahili na mwandiko uwe mgumu kusomeka, lakini watoto watajifunza somo kubwa sana kwa kufanya hivyo.
(3) Ustahimilivu. Sisi sote tumezaliwa na mwelekeo wa ubinafsi, na unaweza kutuzuia kuonyesha shukrani. (Mwanzo 8:21; Mathayo 15:19) Lakini, Biblia inawahimiza watumishi wa Mungu hivi: “Mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu, na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.”—Waefeso 4:23, 24.
Hata hivyo, wazazi wenye uzoefu wanajua kwamba kuwasaidia watoto “kuvaa utu mpya” si jambo rahisi. Stephen, aliyetajwa awali, anasema, “Ni kama ilituchukua muda mrefu sana kuwafundisha binti zetu kusema asante bila kulazimishwa.” Lakini Stephen na mke wake hawakufa moyo. “Kwa ustahimilivu mwingi,” Stephen anaendelea, “wasichana wetu walijifunza kufanya hivyo. Sasa tunafurahi kuwaona wakiwashukuru watu.”
Namna Gani Marafiki na Majirani?
Tunapokosa kusema asante, huenda isiwe kwa sababu hatuna shukrani, labda tu tunasahau. Je, ni muhimu sana kwetu kuonyesha shukrani badala tu ya kuhisi kwamba tumethamini jambo? Ili kujibu swali hilo, fikiria tukio linalomhusu Yesu na wakoma fulani.
Alipokuwa akielekea Yerusalemu, Yesu alikutana na wanaume kumi wenye ukoma. Biblia inaeleza hivi: “Wakapaaza sauti zao na kusema: ‘Yesu, Mwalimu, tuhurumie!’ Naye alipowaona akawaambia: ‘Nendeni mkajionyeshe kwa makuhani.’ Basi walipokuwa wakienda zao wakatakaswa. Mmoja wao, alipoona amepona, akarudi, akimtukuza Mungu kwa sauti kubwa. Naye akaanguka kifudifudi miguuni pa Yesu, akamshukuru; tena, alikuwa Msamaria.”—Luka 17:11-16.
Je, Yesu alipuuza kwamba wale wengine hawakuonyesha shukrani? Simulizi linaendelea kusema: “Yesu akajibu akasema: ‘Wale kumi walitakaswa, sivyo? Basi, wako wapi wale wengine tisa? Je, hawakupatikana wowote waliorudi kumpa Mungu utukufu ila mtu huyu wa taifa lingine?’”—Luka 17:17, 18.
Wale wakoma wengine tisa hawakuwa waovu. Mapema, walikuwa wameonyesha waziwazi kwamba walikuwa na imani katika Yesu na walikuwa tayari kutii maagizo yake ambayo yalitia ndani kusafiri kwenda Yerusalemu ili kujionyesha mbele ya makuhani. Hata hivyo, ingawa bila shaka walithamini sana tendo la Yesu la fadhili, hawakumwonyesha uthamini huo. Jambo hilo lilimkatisha Kristo tamaa. Namna gani sisi? Mtu anapotutendea jambo zuri, je, sisi tunasema asante na, inapofaa, tunaonyesha uthamini kwa kutuma ujumbe ulioandikwa?
Biblia inasema kwamba ‘upendo haukosi adabu, hautafuti faida yake binafsi.’ (1 Wakorintho 13:5BHN) Kwa hiyo, kuonyesha uthamini kwa unyoofu si ishara tu ya adabu bali pia ni uthibitisho wa upendo. Kama tukio kuhusu wakoma linavyotufundisha, wale wanaotaka kumpendeza Kristo wanapaswa kuwaonyesha watu wote upendo na uthamini kama huo, haidhuru taifa, rangi, au dini yao.
Jiulize, ‘Mara ya mwisho ni lini nilipomwambia asante jirani, mfanyakazi mwenzangu, mwanafunzi mwenzangu, mfanyakazi wa hospitali, mwenye duka, au mtu mwingine aliyenisaidia?’ Mbona usiweke rekodi kwa siku moja au mbili na uandike mara ambazo umesema asante au kuandika ujumbe wa shukrani? Rekodi kama hiyo inaweza kukusaidia kuonyesha uthamini zaidi.
Bila shaka, Yehova Mungu ndiye anayestahili zaidi shukrani zetu. Yeye ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yakobo 1:17) Ni lini mara ya mwisho ulipomshukuru Mungu kikweli kwa ajili ya mambo hususa ambayo amekufanyia?—1 Wathesalonike 5:17, 18.
Kwa Nini Uonyeshe Uthamini Hata Wengine Wasipouonyesha?
Huenda watu wengine wasituonyeshe uthamini hata tunapowaonyesha. Basi kwa nini tuwashukuru wengine wasipotushukuru? Fikiria sababu moja tu.
Kwa kuwatendea mema wale wasioonyesha uthamini, tutakuwa tukimwiga Muumba wetu mwenye neema, Yehova Mungu. Hata watu wengi wasipothamini upendo ambao Yehova anaonyesha hilo halimfanyi aache kuwatendea mema. (Waroma 5:8;1 Yohana 4:9, 10) Yeye “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” Tukijitahidi kuonyesha uthamini ijapokuwa tunaishi katika ulimwengu usio na shukrani, tutathibitisha kwamba sisi ni “wana wa Baba [yetu] aliye mbinguni.”—Mathayo 5:45.