Recent Posts

PropellerAds

Friday, August 31, 2018

Maneno Yetu Yanafunua Nini?

Image result for your word
Linda Moyo Wako
“Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.”—MITHALI 4:23.
 Kwa nini tunahitaji kulinda moyo wetu?
MZEE mmoja kwenye kisiwa cha Karibea alitoka mahali alipokuwa amejikinga na kimbunga. Alipotazama uharibifu uliokuwa umetokea mahali hapo, aliona kwamba mti mmoja mkubwa sana ambao ulikuwa umesimama kwa miaka mingi karibu na lango lake la mbele, ulikuwa umetoweka. ‘Imekuwaje hivyo,’ akajiuliza, ‘hali miti midogo zaidi karibu na mti huo ilibaki?’ Alipotazama kisiki cha mti huo alijua sababu. Sehemu ya ndani ya mti huo ulioonekana kana kwamba hauwezi kutikiswa ilikuwa imeoza, na kimbunga kilikuwa kimefichua tu kuoza huko.
 Inasikitisha kama nini wakati mwabudu wa kweli anayeonekana kuwa Mkristo thabiti anaposhindwa na jaribu la imani! Kwa kufaa, Biblia inasema kwamba “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwanzo 8:21) Hiyo yamaanisha kwamba hata mioyo iliyo mizuri inaweza kushawishiwa kufanya mabaya tusipoendelea kuwa macho. Kwa kuwa moyo usiokamilika wa mwanadamu unaweza kupotoshwa, tunahitaji kuchukua kwa uzito ushauri huu: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo.” (Mithali 4:23) Tunaweza kulinda moyo wetu wa mfano jinsi gani?
Ni Muhimu Kujichunguza Mara kwa Mara
. (a) Ni maswali gani yanayoweza kuulizwa kuhusiana na moyo halisi? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuchunguza moyo wetu wa mfano?
 Ukienda kumwona daktari ili kufanyiwa uchunguzi, yaelekea atachunguza moyo wako. Je, afya yako kwa ujumla, kutia ndani moyo wako, inaonyesha kwamba unapata chakula chenye lishe ya kutosha? Shinikizo la damu yako likoje? Je, moyo wako unapiga kwa njia ya kawaida? Je, unafanya mazoezi ya kutosha? Je, moyo wako unapata mkazo mwingi kupita kiasi?
Ikiwa moyo halisi unahitaji kuchunguzwa kwa ukawaida, vipi moyo wako wa mfano? Yehova huuchunguza. (1 Mambo ya Nyakati 29:17) Sisi pia tunapaswa kufanya vivyo hivyo. Jinsi gani? Kwa kuuliza maswali kama haya: Je, moyo wangu hupata chakula cha kiroho cha kutosha kupitia funzo la kibinafsi la ukawaida na kuhudhuria mikutano? (Zaburi 1:1, 2; Waebrania 10:24, 25) Je, moyo wangu unafikiria sana ujumbe wa Yehova kama “moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu,” ukinichochea kushiriki kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi? (Yeremia 20:9; Mathayo 28:19, 20; Warumi 1:15, 16) Je, ninachochewa kujikakamua kisulubu kushiriki katika aina fulani ya huduma ya wakati wote inapowezekana? (Luka 13:24) Ninaruhusu moyo wangu wa mfano upatwe na mambo gani? Je, ninajitahidi kushirikiana na wengine ambao mioyo yao imeungamanishwa katika ibada ya kweli? (Mithali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Na tuwe wepesi kutambua udhaifu wowote ule katika moyo wetu na kuchukua hatua mara moja kurekebisha jambo hilo.
 Majaribu ya imani yanaweza kutimiza kusudi gani lenye manufaa?
Mara kwa mara sisi hupatwa na majaribu ya imani. Majaribu hayo yanatuwezesha kujua hali ya moyo wetu. Musa aliwaambia hivi Waisraeli waliokuwa karibu kuingia katika Bara Lililoahidiwa: ‘BWANA, Mungu wako alikuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo.’ (Kumbukumbu la Torati 8:2) Tunapokabili hali tusizotarajia au majaribu, je, mara nyingi hatushangazwi na hisia na tamaa tunazoonyesha, au jinsi tunavyotenda? Majaribu ambayo Yehova huruhusu yatupate yanaweza kwa hakika kutusaidia kutambua kasoro zetu na hivyo kujirekebisha. (Yakobo 1:2-4) Na tusikose kamwe kutafakari na kusali kuhusu jinsi tutendavyo tunapopatwa na majaribu!
Maneno Yetu Yanafunua Nini?
 Mambo tunayopenda kuzungumzia yanaweza kufunua nini kuhusu moyo wetu?
Tunawezaje kujua mambo tuliyoweka hazina moyoni mwetu? Yesu alisema: “Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutokeza ambayo ni maovu katika hazina yake mbovu; kwa maana katika wingi wa moyo kinywa chake husema.” (Luka 6:45) Yale tunayozungumzia kwa ukawaida huonyesha vizuri yale ambayo moyo wetu umeazimia kufanya. Je, mara nyingi sisi huzungumza juu ya vitu vya kimwili na mafanikio ya kilimwengu? Au je, mara nyingi mazungumzo yetu hukazia mambo ya kiroho ? Badala ya kuzungumza kuhusu makosa ya wengine, je, tuna mwelekeo wa upendo wa kuyafunika? (Mithali 10:11, 12) Je, tuna mwelekeo wa kuzungumza sana kuhusu watu na shughuli zao maishani, huku tukizungumza machache kuhusu mambo ya kiroho na ya kiadili? Je, hiyo inaweza kuwa ishara kwamba tunajiingiza kupita kiasi katika mambo ya kibinafsi ya wengine?—1 Petro 4:15.
Ni somo gani kuhusu kulinda moyo wetu tuwezalo kujifunza kutokana na masimulizi kuhusu ndugu kumi wa Yosefu?
Fikiria yaliyotokea katika familia moja kubwa. Wana kumi wa Yakobo wenye umri mkubwa ‘hawakuweza kusema kwa amani’ na Yosefu, ndugu yao mdogo. Kwa nini? Walimwonea wivu kwa kuwa alipendwa sana na baba yao. Baadaye Yosefu alipopata ndoto kutoka kwa Mungu zilizoonyesha kwamba alikuwa na kibali cha Yehova, ndugu zake ‘walizidi kumchukia.’ 
(Mwanzo 37:4, 5, 11) Kwa ukatili, walimwuza ndugu yao awe mtumwa. Kisha ili kuficha dhambi yao, wakamhadaa baba yao afikiri kwamba Yosefu alikuwa ameuliwa na mnyama mwitu. Ndugu kumi wa Yosefu walishindwa kulinda moyo wao wakati huo. Ikiwa sisi ni wepesi kuchambua wengine, je, hiyo inaweza kuwa uthibitisho kwamba tuna husuda au wivu moyoni? Tunahitaji kuwa waangalifu kuchunguza kinachotoka vinywani mwetu na kung’oa haraka maelekeo yasiyofaa.
 Ni nini kitakachotusaidia kuchunguza moyo wetu tunaposema uongo?
Ingawa “haiwezekani Mungu kusema uongo,” wanadamu wasiokamilika wana maelekeo ya kusema uongo. (Waebrania 6:18) “Wanadamu wote ni waongo,” akasikitika mtunga-zaburi. (Zaburi 116:11) Hata mtume Petro alisema uwongo mara tatu alipomkana Yesu. (Mathayo 26:69-75) Ni wazi kwamba tunapaswa kuwa waangalifu kuepuka kusema uongo, kwa kuwa Yehova huchukia ‘ulimi wa uongo.’ (Mithali 6:16-19) Iwapo tumesema uongo, lingekuwa jambo la hekima kuchunguza tujue ni nini kilichotufanya tuseme uongo huo. Je, tulifanya hivyo kwa sababu ya kumwogopa mwanadamu? Je, tuliogopa kuadhibiwa? Labda ni kwa sababu tuliona aibu au ni kwa sababu ya ubinafsi tu? Hata sababu iwe nini, inafaa kama nini kutafakari jambo hilo, kukubali kosa letu kwa unyenyekevu, kumwomba Yehova msamaha, na kutafuta msaada wake ili kushinda udhaifu huo! Huenda ikafaa zaidi kutafuta msaada wa “wanaume wazee wa kutaniko.”—Yakobo 5:14.
Sala zetu zinaweza kufunua nini kuhusu moyo wetu?
Yehova alisema hivi akijibu ombi la Mfalme Solomoni mchanga la kuwa na hekima na ujuzi: “Kwa sababu neno hili lilikuwamo moyoni mwako, wala hukujitakia mali, wala utajiri, wala utukufu . . . , basi hekima na maarifa umepewa; nami nitakupa mali, na utajiri, na utukufu.”
 (2 Mambo ya Nyakati 1:11, 12) Yehova alijua yaliyokuwamo moyoni mwa Solomoni kutokana na yale aliyoomba na yale ambayo hakuomba. Mazungumzo yetu na Mungu yanafunua nini kuhusu moyo wetu? Je, sala zetu zinaonyesha kwamba tunataka sana kupata ujuzi, hekima, na ufahamu? 
(Mithali 2:1-6; Mathayo 5:3) Je, masilahi ya Ufalme yamo moyoni mwetu? (Mathayo 6:9, 10) Ikiwa tunasali bila kufikiri au kidesturi tu, jambo hilo laweza kudhihirisha uhitaji wa kuchukua wakati wa kutafakari matendo ya Yehova.
 (Zaburi 103:2) Wakristo wote wanapaswa kuwa macho kutambua sala zao zinafunua nini.
Matendo Yetu Yanafunua Nini?
 (a) Uzinzi na uasherati huanzia wapi? (b) Ni nini kitakachotusaidia ‘tusifanye uzinzi moyoni’?
 Imesemekana kwamba muungwana ni kitendo. Matendo yetu hufunua mengi sana kuhusu hisia zetu za ndani. Kwa mfano, kuhusiana na maadili, kulinda moyo huhusisha mengi zaidi ya kuepuka tu tendo la uasherati au uzinzi. Yesu alisema hivi kwenye Mahubiri yake ya Mlimani: “Lakini mimi nawaambia: ye yote atakayemwangalia mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Tunaweza kuepuka kwa njia gani kufanya uzinzi hata katika moyo wetu?
Mzee wa ukoo AYubu aliwawekea kielelezo wanaume na wanawake Wakristo waliofunga ndoa. Hapana shaka kwamba Yobu alikutana na wanawake wachanga katika shughuli zake za kila siku, na hata kuwasaidia kwa fadhili walipohitaji msaada. Lakini Yobu, mtu mwenye uaminifu-maadili, hakujiruhusu avutiwe nao kimapenzi. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa ameazimia kabisa kutowatazama wanawake kwa kuwatamani. “Nilifanya agano na macho yangu,” akasema. “Basi nawezaje kumwangalia msichana?” 
(Ayubu 31:1) Na tufanye agano kama hilo na macho yetu na kulinda moyo wetu.
 Unaweza kutumia andiko la Luka 16:10 jinsi gani kuhusiana na kulinda moyo wako?
 Mwana wa Mungu alisema: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni asiye mwaminifu katika lililo kubwa pia.” 
(Luka 16:10) Naam, tunahitaji kuchunguza mwenendo wetu kuhusiana na mambo yanayoonekana kuwa madogo ambayo sisi hufanya kila siku, hata yale ambayo sisi hufanya nyumbani mwetu.
 (Zaburi 101:2) Tunapoketi nyumbani mwetu tukitazama televisheni, au kutumia Internet, je tunakuwa waangalifu kufuata ushauri huu wa Kimaandiko: “Acheni uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata visitajwe hata miongoni mwenu, kama vile ifaavyo watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maongezi ya kipumbavu wala kufanya mzaha wenye aibu, mambo yasiyofaa”? (Waefeso 5:3, 4) Namna gani jeuri tunayoweza kutazama kwenye televisheni au katika michezo ya video? “Yehova huchunguza mwadilifu na mwovu pia, na nafsi Yake humchukia yeyote apendaye jeuri,” akasema mtunga-zaburi.—Zaburi 11:5.
Tunahitaji kuwa na tahadhari gani tunapotafakari yale yatokayo moyoni mwetu?
Yeremia alionya: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha.” (Yeremia 17:9) Udanganyifu huo wa moyo unaweza kuonekana tunapojitetea au kupunguza uzito wa makosa yetu, kupuuza kasoro zetu mbaya, au kutia chumvi mafanikio yetu. Moyo wenye ugonjwa wa kufisha unaweza pia kuwa mnafiki—useme mambo yenye kupendeza, na kutenda kinyume. (Zaburi 12:2; Mithali 23:7) Ni muhimu kama nini kuwa wanyofu tunapochunguza yale yatokayo moyoni mwetu!
Je, Jicho Letu Ni Sahili?
(a) Jicho “sahili” ni nini? (b) Kudumisha jicho letu likiwa sahili hutusaidia jinsi gani kulinda moyo?
14 Yesu alisema, “Taa ya mwili ni jicho.” Kisha akaongeza: “Basi, ikiwa jicho lako ni sahili, mwili wako wote utakuwa mwangavu.” (Mathayo 6:22) Jicho lililo sahili hukazia uangalifu mradi au kusudi moja bila kukengeushwa. Naam, jicho letu lapaswa kukazia uangalifu “kutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].” (Mathayo 6:33) Ni nini kiwezacho kuupata moyo wetu wa mfano ikiwa jicho letu si sahili?
 Fikiria hali ya kupata riziki. Kuiruzuku familia yako ni takwa la Kikristo. (1 Timotheo 5:8) Lakini namna gani iwapo tunashawishiwa na tamaa ya kuwa na vitu vya kisasa, vilivyo bora zaidi, na vinavyopendwa zaidi, kama vile chakula, mavazi, makao, na vitu vinginevyo? Je, kweli hali hiyo haitatawala moyo na akili, ikifanya ibada yetu iwe ya moyo nusu nusu? (Zaburi 119:113; Warumi 16:18) Mbona tujishughulishe sana na mahitaji ya kimwili hivi kwamba katika maisha yetu tunafikiria tu familia, biashara, na vitu vya kimwili? Kumbuka ushauri huu uliopuliziwa: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe kwamba mioyo yenu isiwe kamwe yenye kulemewa na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara hiyo kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wote wale wanaokaa juu ya uso wa dunia yote.” —Luka 21:34, 35.
 Yesu alitoa ushauri gani kuhusu jicho, na kwa nini?
Jicho ni kiungo muhimu sana kwa kuwa linawasilisha habari katika akili na moyo. Mambo linalotazama yanaweza kuathiri sana mawazo, hisia, na matendo yetu. Kwa kutumia lugha ya mfano, Yesu alitaja jinsi macho yalivyo kishawishi chenye nguvu: “Ikiwa, sasa, jicho lako hilo la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe kabisa na ulitupilie mbali nawe. Kwa maana ni manufaa zaidi kwako kimoja cha viungo vyako kipotee kwako kuliko mwili wako wote kutupwa katika jehanamu.” (Mathayo 5:29) Jicho lapaswa kuzuiwa lisitazame mambo yasiyofaa. Kwa mfano, halipaswi kuruhusiwa kutazama habari ambayo imekusudiwa kusisimua au kuamsha hamu na tamaa zisizofaa.
 Kufuata andiko la Wakolosai 3:5 hutusaidia jinsi gani kulinda moyo?
Mbali na macho, kuna njia nyinginezo za kupata habari. Uwezo wa kugusa na kusikia hutumika pia, na tunahitaji kuchukua hatua za tahadhari kuhusiana na viungo vingine vinavyohusika. Mtume Paulo alishauri: “Fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa, ambako ni ibada ya sanamu.”Wakolosai 3:5.
Twapaswa kuchukua hatua gani kuhusiana na mawazo yasiyofaa?
Tamaa isiyofaa yaweza kutoka katika sehemu ya ndani kabisa ya akili yetu. Kwa kawaida, kuwaza sana juu ya tamaa isiyofaa hufanya iongezeke na kuathiri moyo. “Kisha tamaa, wakati imetungika mimba, huzaa dhambi.” (Yakobo 1:14, 15) Wengi hukiri kwamba hivyo ndivyo mara nyingi mtu huanza kupiga punyeto. Ni muhimu kama nini kuendelea kujaza akili yetu mambo ya kiroho! (Wafilipi 4:8) Wazo lisilofaa likiingia akilini mwetu, twapaswa kujitahidi kuliondoa.
‘Tumikia Mungu kwa Moyo Wako Wote’
 Tunaweza kufanikiwaje kumtumikia Yehova kwa moyo wote?
Alipokuwa mzee, Mfalme Daudi alimwambia hivi mwanawe: “Solomoni mwanangu, umjue Mungu wa baba yako, na umtumikie kwa moyo wako wote na kwa nia thabiti; yeye Mwenyezi-Mungu huchunguza mioyo na anafahamu mipango na fikira za binadamu.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9,) Solomoni mwenyewe alisali apewe “moyo mtiifu.” (1 Wafalme 3:9, ) Hata hivyo, haikuwa rahisi kwake kudumisha moyo huo katika maisha yake yote.
 Ili tufanikiwe kumtumikia Yehova kwa moyo wote, ni lazima tujipatie moyo unaompendeza na kuulinda pia. Ili kufanya hivyo, ni lazima tuviweke moyoni vikumbusho vya Neno la Mungu—‘kuvihifadhi ndani ya moyo.’ (Mithali 4:20-22) Pia twapaswa kuwa na mazoea ya kuchunguza moyo wetu, na kutafakari kwa sala yale yanayofichuliwa na maneno na matendo yetu. Kutafakari huko hakutakuwa na matokeo tusipotafuta kwa bidii msaada wa Yehova ili kusahihisha udhaifu wowote tunaotambua. Ni muhimu kama nini kuwa waangalifu sana kuhusiana na yale tunayoingiza moyoni mwetu kupitia hisi zetu! Kwa kufanya hivyo, tunahakikishiwa kwamba “amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Naam, na tuazimie kulinda moyo wetu kuliko yote tuyalindayo na kumtumikia Yehova kwa moyo wote.
Je, Unakumbuka?
• Kwa nini ni muhimu kulinda moyo?
• Kuchanganua yale tunayosema hutusaidia jinsi gani kulinda moyo wetu?
• Kwa nini tudumishe jicho letu likiwa “sahili”?
Tafadhali tutumie barua pepe kwa Ushauri na Maombi Email: jagaji61@gmail.com