Recent Posts

PropellerAds

Friday, April 28, 2017

Sheria za Ubongo: Kanuni kumi na mbili za kukuongoza katika sehemu yako ya kazi au Shuleni


Na: Amani manamba

1.  Kuna uhusiano mkubwa kati ya mazoezi na utayari wa akili kufanya kazi. Mwandishi anatushirikisha kuwa mwili wa mwanadamu umeumbwa kiasi kwamba unaweza kutembea maili 12 kwa siku. Katika mzunguko huo mwili unaweza kufanya kazi mbalimbali ambazo zinatofautisha dunia ya kizazi kimoja hadi kingine. Kwa ujumla unaweza fupisha maana hii kwa kutumia maneno haya “wakakamavu ndo wanaishi – survivor of the fittest”. Ukweli huu unadhihirishwa na maendeleo ya mwanadamu toka enzi za kutegemea asili (matunda na mizizi) mpaka kuwa mzalisha na mboreshaji wa mazingira. Hii yote ni kazi ya ubongo ambayo imefanikisha uwepo wa vifaa vya kurahisisha utendaji kazi na mawasiliano.

2.  Mazoezi ni njia mojawapo ya kumwezesha mtu kuishi maisha marefu. Mwili uliojengeka kwa mazoezi ni nadra sana kushambuliwa na magonjwa nyemerezi, hivyo, kama unahitaji kuishi maisha marefu huna budi kuishi maisha ya mazoezi kwa ajili ya uimara wa mwili pamoja na akili. Jibu la ukweli huu ni rahisi kwa kadri unavyofanya mazoezi ndivyo unaifanya misuli iwe imara na hivyo kupelekea kupunguza hatari ya magonjwa ya moyo. Pia, utafiti unaonesha kuwa watu ambao wameishi maisha ya mazoezi wana faida ya kuwa na utimamu wa akili kwa muda mrefu na hivyo ni rahisi kwao kufikiria na kuchanganua mambo haraka. Mazoezi yanapunguza hatari ya kupatwa na magonjwa kwa kiwango cha zaidi ya 60%.

3.  Mazoezi yanasaidia kuimarisha afya ya watoto. Mwandishi anatushirikisha kuwa watoto ambao wanajihusisha na mazoezi wana afya bora ikilinganishwa na watoto wanaofungiwa ndani muda wote. Kadri watoto wanavyokuwa na afya imara ndivyo inakuwa rahisi kufanya vyema katika masomo yao. Hii ni kutokana na ukweli kwamba watoto ambao ni wakakamavu mara nyingi huwa na afya imara, wasikivu na wanaojiamini katika yale wanayofanya.

4.   Ubongo ni asilimia 2 tu ya sehemu yote ya mwili wa binadamu lakini sehemu hii inatumia karibia asilimia 20 ya nishati yote inayohitajika na mwili. Njia pekee ya kufanikisha seli za mwili ziendelee kufanya kazi yake zikiwemo seli za ubongo ni mzunguko wa damu kuendelea kusambaa sehemu zote za mwili. Kadri unavyofanya mazoezi unawezesha damu iweze kuzunguka haraka na kwa kasi na hivyo kufanikisha usambazaji wa hewa ya oksijeni pamoja na kuondoa sumu kwa njia ya jasho.

5.  Kuna njia mbili za kukabiliana na changamoto za mazingira yetu. Njia ya kwanza ni kuwa na nguvu zaidi na njia ya pili ni kuwa na uwelevu/akili zaidi. Njia ya pili ni nzuri zaidi kwa vile inatuwezesha kutawala ulimwengu huu kwa kutumia nguvu kidogo huku tukitumia ubongo wetu. Na hii ndiyo njia pekee inayotutofautisha sisi pamoja na viumbe wenye ukaribu na sisi kama vile Gorila. Uwezo wa kuchanganua mambo kwa kutumia picha ya vitu husika akilini mwetu ni nyenzo muhimu ambayo imeendelea kutofautisha kizazi cha mwanadamu na viumbe wengine na ni kupitia uwezo huu mwanadamu ameendeleza uumbaji wa kila aina kwa ajili ya kuboresha utendaji kazi katika mazingira yanayomzunguka.

6.  Ubongo ni kiumbe hai na hivyo unahitaji haki zote za kuwa hai ili uendelee kuishi. Haki kubwa kabisa ya kuwa hai si nyingine zaidi ya kuhitaji kuboreshwa kutoka chini kwenda juu kithamani (evolution) kupitia kwenye sheria ya asili ya kuchagua.  Kiumbe yeyote anayeishi ni lazima apate chakula baada ya kula ili kiumbe huyo aendelee kuwepo siku zijazo ni lazima pawepo kuzaliana kwa ajili ya kupitisha tabia moja kwenda kizazi kingine. Hivi ndivyo ubongo wa mwanadamu umekuwa ukiendelea kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Hapa utagundua kuwa ubongo unaboreshwa kutoka kwenye ubongo wa kutegemea asili mpaka kufikia kwenye ubongo wa kutaka kuishi mwezini.

7.  Kutokana na mfumo wa ubongo kusukwa tofauti ndiko kunapelekea watu wawe na vipaji tofauti. Ndiyo maana utakuta kuna mchezaji kama Christiano Ronaldo ambaye amefanikiwa katika soka lakini ukimpeleka katika mpira wa kikapu hawezi kufikia mafanikio ya Michael Jordan. Mwandishi anatushirikisha kuwa huu ni ukweli ambao unatofautisha kazi za uumbaji wa vitu kati mwanadamu mmoja na mwingine. Habari njema ni kwamba ubongo unaweza mfumo wa ubongo unaweza kusukwa upya kutokana na mazoea ya kazi unayofanya. Ni kutokana na ukweli huu mwanadamu anahimarika kila siku kutokana na kazi ambayo amezoea kuifanya mara kwa mara kwa vile ubongo unazoea kile ambacho kinafanyika mara kwa mara.

8.  Seli za ubongo ndani mwake zina vinyuzi vidogo ambavyo uitwa neurons. Vinyuzi hivi vinafanya kazi sawa na nyaya za umeme ambapo katika mfumo wa ubongo vinasaidia kusafirisha taarifa moja kutoka kwenye ubongo kwenda kwenye viungo vingine vya mwili. Kabla ya taarifa kutumwa kwenye viungo vya mwili ni lazima kwanza ubongo uzitafsri na ndipo unaagiza sehemu ya mwili husika kuchukua hatua. Ubongo unafanya kazi kiasi ambacho unaweza kufanyia kazi taarifa moja na kuacha nyingine kwa kutegemea matokeo tarajiwa kwa taarifa husika. Hapa unatakiwa kujenga utamaduni wa kuufundisha ubongo wako kufanyia kazi taarifa zenye matokeo chanya tu.

9.  Ubongo ni sawa na msuli kwa maana ya kwamba kadri unavyotumiwa mara kwa mara ndivyo unaimarika zaidi. Ni mara nyingi tumeona namna ambavyo watu wenye mazoezi wanavyokuwa na misuli iliyotuna zaidi ikilinganishwa na watu wengine. Na mfumo wa utendaji kazi wa ubongo ndivyo ulivyo kwa maana ya kwamba kadri unavyotumiwa zaidi ndivyo unaimarika zaidi kwa kuongeza uwezo wa kufikri na kuchanganua mambo kwa haraka. Hivyo ni lazima uwe tayari kuufundisha ubongo wako kufikria njee ya boksi.

10.  Kadri ubongo unavyotumia muda mwingi kwenye kichochezi au chanzo cha taarifa ndivyo taarifa husika itatafsiriwa na kufanyiwa kazi na hatimaye kujidhihirisha kwenye ulimwengu wa nje. Hii ni sifa inayopelekea ufanisi wa ubongo kufanikisha mambo mapya kupitia kujifunza mara kwa mara. Kwa sifa hii kila mtu anaweza kuwa ufanisi katika kila sekta ya maisha yake kwa kutumia muda mwingi kufikiria na kujifunza yale ambayo yana umuhimu katika kufikia mafanikio anayokusudia.

11.  Mara nyingi vipaumbele vyetu vinatokana na kumbukumbu, hobi pamoja na ufahamu wetu. Tunatumia historia kuhisi namna ambavyo tunaweza kufanikisha matokeo yale tunayowaza. Kwa ufupi ni kwamba kila aina ya mazingira tuliyozoea yana mchango katika matukio ya maisha yetu ya kila siku. Pia, tamaduni na makuzi tuliyokulia yana nafasi kubwa ya kutambulisha jinsi tulivyo katika kudhibiti hisia zetu.

12.  Ubongo unaweza kufanyia kazi moja kwa ufasaha na kutoa jibu moja kati ya zuri au baya na si vyote kwa pamoja. Hapa mwandishi anatufundisha kuwa neurons za ubongo zinafanya kazi katika mfumo unaotoa matokeo ya upande mmoja kwa wakati husika pasipo kujali kama wema au ubaya wa matokeo husika. Kwa maana hii, tunafundishwa kuwa hatuwezi kuwa wenye furaha na huzuni kwa wakati mmoja, hatuwezi kukimbia na kutembea  kwa wakati mmoja au hatuwezi kuwa hofu na kujiamini kwa wakati mmoja. Ni lazima tukio moja lipewe nafasi kwa wakati husika badala ya tukio kinzani.

13.  Hisia zinawezesha ubongo kujifunza. Hapa mwandishi anatufundisha kuwa hisia ni chanzo cha ubongo kujifunza na hivyo hisia zetu ndo zinaamua ni wapi akili zetu zimejikita zaidi katika maisha yetu ya kila siku.

14.  Ubongo una sehemu maalum kwa ajili ya kutunza kumbukumbu ya matukio. Mwandishi anatufundisha kuwa yale yanayopewa kipaumbele kwa kurudiwa mara kwa mara katika maisha ya muhusika ni rahisi sana kukumbukwa na hatimaye kuwa desturi ya maisha ya kila siku. Kwa maana hii ni wazi kuwa imani yetu katika vitu au matukio kwenye ulimwengu huu ni matokeo ya kujifunza sisi wenyewe au kufundishwa kutoka kwa watu wengine wanaotuzunguka. Hii ni kutokana na ukweli kwamba tulikuja ulimwenguni humu tukiwa watupu kwa maana ya ubongo wetu ulikuwa wazi japo kadri umri ulivyosogea ndivyo tulijifunza au kufundishwa zaidi juu ya mema au mabaya ya dunia hii.
15.  Kumbukumbu ni nyenzo muhimu ya kuboresha maisha ya mwanadamu. Nyenzo hii inashikilia mahusiano, maarifa na uchumi wa kila mwanadamu kutokana na ukweli kwamba kumbukumbu inamwezesha mwanadamu hasipotezee muda wa kurudia kujifunza kila siku matukio ambayo yamekuwepo toka mwanadamu aumbwe. Hapa mwandishi anatukumbusha kuwa pasipo kuwa na kumbukumbu imara ni lazima muhusika ajikute kwenye hali ya kurudia makosa yale yale kila mara.

16.  Taarifa nyingi zinazoingia kwenye ubongo sehemu kubwa hazifanyiwa kazi na hivyo zinasahaulika ndani ya muda mfupi na zile ambazo zinapewa kipaumbele zina nafasi ya kukumbukwa. Njia pekee ya kuepuka kupoteza taarifa muhimu ni kujenga utamaduni wa kutembea na kijitabu kidogo kwa ajili ya kuhifadhi taarifa muhimu ili ziendelee kupewa kipaumbele zaidi. Hapa mwandishi anatushirikisha kuwa hauwezi kurudia kitu ambacho hauna kumbukumbu zake hivyo ni muhimu kuimarisha mfumo wa kumbukumbu.

17.  Usingizi ni sehemu ya kupumzisha na ubongo kwa ajili ya kutoa nafasi ya kufikiria vyema zaidi. Pale tunapolala sio kwamba ubongo nao unalala bali unapunguziwa majukumu kwenye baadhi ya viungo vya mwili. Tendo hili linatoa nafasi kwa ubongo kufikiri vyema na hii inatoa nafasi kwa ubongo kutunza nguvu kwa ajili ya kazi ya baadae. Katika muda huu wa mapumziko neurons zinapata nafasi ya kurudia matukio ya mkanda wa matukio yote kwa siku husika. Hivyo ni wazi kuwa unapokosa muda wa kutosha kwa ajili ya usingizi ndivyo na ufanisi wako wa kufikiri na kutenda kazi unavyokuwa duni.

18.  Ubongo wenye msongo wa mawazo hauwezi kujifunza kwa urahisi. Ufanisi katika masomo au utendaji kazi unatofautiana kati ya mtu mwenye msongo wa mawazo na yule ambaye yuko huru. Pia, msongo wa mawazo unaweza pelekea matatizo ya moyo kushindwa kufanya kazi yake kwa ufasaha.

19.  Watu wengi katika jamii ya sasa wanakosa muda wa kutoa malezi bora kwa watoto wao kwa vile wanabanwa na majukumu ya kazi zao. Kwa ujumla watoto wanajikuta katika hali ya msongo wa mawazo kwa vile watu wa kuwapa ushauri hawako karibu nao muda mwingi. Kadri msongo wa mawazo unavyozidi kwa watoto hawa matokeo yake ni kwamba ubongo wao unajazwa na hofu, vitu hasi, hasira, visasi na hatimaye ubongo wa namna hii una ubunifu wa chini sana.

20.  Mwanafunzi wa kwanza kabisa ambaye anatakiwa kupewa nafasi ya kujifunza ni mzazi. Mwandishi anatushirikisha kuwa elimu ya sasa inamlenga mtoto wa kuanzia miaka mitano au sita. Katika umri kama huu mtoto anapofika shuleni anakutana na mwalimu ambaye ni mpya kabisa katika mazoea ya mtoto, hali hii inaweza kumfanya mtoto hasiwe na mafanikio kama hana msingi mzuri wa malezi kutoka kwa wazazi. Hivyo, kama mzazi ni lazima ujifunze mara kwa mara namna ambavyo utamjenga mwanao katika maisha ya kujiamini katika kila hali inayomzunguka.

21.  Tumia milango yako yote ya fahamu katika kila tukio linalokukabili. Mfano, tumia masikio kusikia, macho kuona, ngozi kuhisi, pua kunusa na ikibidi ulimi kuonja pindi unapochanganua hali ya tukio. Milango hii ya fahamu kila mmoja kwa mfumo wake wa neurons unatuma taarifa kwenye ubongo na hatimaye ubongo kwa haraka unatafsiri tukio husika kwa pamoja. Kwa vile ubongo unatafsiri taarifa kwa kutegemea uzoefu wa muhusika hivyo taarifa moja inaweza kuwa tafsiri mbili tofauti kwa watu wawili. Hapa tunajifunza kuwa njia bora ya kujifunza kwa urahisi ni kuhakikisha tunahusisha milango yetu yote ya fahamu kwa ajili kumbukumbu zaidi.

22.  Ni rahisi sana kujifunza kwa kutumia picha kuliko maneno. Ubongo unajifunza mengi kutokana na mchoro au picha kuliko ilivyo kwenye maneno. Mwandishi anatushirikisha kuwa hatuna budi ya kutengeneza mchoro au picha akilini mwetu juu ya yale tunayowaza au kutamani katika maisha yetu. Picha inaleta uhalisia wa kitu au tukio katika ulimwengu wa nje. Kwa maana hii mfumo wa fahamu wa kuona ni mfumo mama ambao unaweza kuutumia kuamsha mifumo ya fahamu mingine.

23.  Binadamu ameumbwa katika hali ambayo inampendelea kuitawala dunia hii. Hii ni kutokana na ukweli kwamba mfumo wa ubongo unamwezesha kila mmoja kujifunza vitu vipya na kutumia vitu hivi katika maisha yake ya kila siku. Kwa maana hii tunaweza kujifunza vitu vipya au kuboresha vitu vipya kwa kutumia neurons za ubongo.