Recent Posts

PropellerAds

Saturday, April 16, 2016

Barabara ya kwanza ya juu kujengwa Dar-es- Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John
Pombe Magufuli ameweka jiwe la msingi la mradi wa
ujenzi wa barabara ya juu (Flyover) katika makutano
ya barabara ya Nyerere na Mandela, eneo la Tazara
Jijini Dar es salaam ambayo inatarajiwa kukamilika
ifikapo Oktoba 2018.
Sherehe ya uzinduzi wa mradi huo imefanyika kando ya
eneo la makutano ya barabara ya Nyerere na Mandela
Jijini Dar es salaam, ambapo pamoja na Rais Magufuli
aliyeongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli,
imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo
Mawaziri, Wabunge, Mameya wa Jiji la Dar es salaam
na Balozi wa Japan hapa nchini Mheshimiwa Masaharu
Yoshida.
Barabara hiyo ya juu itakuwa ya kwanza kujengwa hapa
nchini na ujenzi wake umepangwa kugharimu takribani
shilingi Bilioni 100 ambapo kati ya fedha hizo shilingi
Bilioni 93.44 zitatolewa na Japan kupitia Shirika lake
la Ushirikiano wa Kimataifa (JICA), na Serikali ya
Tanzania itatoa shilingi Bilioni 8.3.
Barabara ya juu itakayojengwa itakuwa na njia nne na
urefu wa mita 300 kutokea maeneo ya katikati ya Jiji
la Dar es salaam kuelekea uwanja wa ndege wa
Kimataifa wa Julius Nyerere, na inatarajiwa kupunguza
kero ya msongamano wa magari yaendayo na yatokayo
Uwanja wa ndege na Bandari ya Dar es salaam.
Akizungumza kabla ya kuweka jiwe la msingi la mradi
huo, Rais Dkt. John Pombe Magufuli amesema
barabara hiyo inajengwa ikiwa ni utekelezaji wa ahadi
ya serikali yake ya kumaliza tatizo la msongamano wa
magari Jijini Dar es salaam, ambao kwa mwaka 2013
pekee utafiti umeonesha ulisababisha upotevu wa shilingi
Bilioni 411.55
Rais Magufuli amebainisha juhudi nyingine za kukabiliana
na msongamano wa magari Jijini Dar es salaam kuwa
ni pamoja na kujenga barabara ya njia sita ya Dar es
salaam hadi Chalinze ambayo itakuwa na Flyover tano,
ujenzi wa barabara nyingine za juu katika makutano ya
barabara za Nelson Mandela, Morogoro na Sam
Nojuma eneo la Ubungo na ujenzi wa daraja jipya la
Salander lenye urefu wa kilometa 6.23 kuanzia Coco
Beach hadi hospitali ya Agha Khan.
Juhudi nyingine ni ujenzi wa awamu ya pili wa
miundombinu ya mabasi yaendayo haraka katika
barabara za Kilwa, Chang'ombe na Kawawa, na ujenzi
wa awamu ya tatu wa miundombinu ya mabasi
yaendayo haraka katika barabara za Nyerere - Gongo
la Mboto na Uhuru - Azikiwe.
Aidha, Rais Magufuli amezungumzia awamu ya kwanza
ya mradi wa mabasi yaendayo haraka, kuwa serikali
yake imelazimika kusimamisha kuanza kwa huduma hiyo
baada ya kubaini dosari katika mkataba wa mradi
ambazo zingesababisha serikali kupoteza fedha nyingi na
wananchi kutwishwa mzigo mzito wa viwango vikubwa
vya nauli, na amewahakikishia wananchi wa Dar es
salaam kuwa mabasi hayo yataanza kutoa huduma hivi
karibuni baada ya kurekebisha kasoro zilizobainika.
Dkt. Magufuli pia amezungumzia usafi wa Jiji la Dar es
salaam kwa kuwataka viongozi wa Manispaa zote za
Jiji, kuhakikisha wanatafuta namna ya kudhibiti utupaji
hovyo wa takataka ikiwemo kutoza faini kubwa kwa
watakaokamatwa wakitupa takataka hovy