Recent Posts

PropellerAds

Thursday, April 28, 2016

Wanaojitambulisha kama walimwengu waongezeka

NchiWatu wengi duniani wanajitambulisha kama raia wa ulimwengu badala ya raia wa nchi zao, utafiti wa maoni uliofanywa na BBC umebaini.
Mtindo huu sana umevuma katika mataifa yanayoinuka kiuchumi ambapo watu wengi wanakumbatia zaidi mtazamo wa kimataifa.
Hata hivyo, kuna watu wachache Ujerumani wanaojihisi kuwa raia wa ulimwengu kwa sasa wakilinganishwa na mwaka 2001.
Kampuni ya kufanya utafiti ya GlobeScan iliwahoji watu zaidi ya 20,000 katika nchi 18.
Zaidi ya nusu ya watu waliohojiwa (56%) katika mataifa yanayoendelea walijitazama kuwa raia wa ulimwengu badala ya raia wa mataifa yao.
Idadi ilikuwa juu sana Nigeria (73%), China (71%), Peru (70%) na India (67%).
Hali inaenda kinyume katika nchi zilizostawi. Idadi ya wanaojitazama kama raia wa ulimwengu ilianza kushuka sana hasa baada ya mgogoro wa kiuchumi uliotokea 2008. Nchini Ujerumani kwa mfano, ni 30% pekee waliojitazama kama raia wa dunia.
Kwa mujibu wa Lionel Bellier kutoka GlobeScan, hiki ndicho kiwango cha chini zaidi kushuhudiwa tangu kuanza kufanywa kwa utafiti huu miaka 15 iliyopita.
"Hili linafaa kutazamwa katika muktadha wa mazingira yaliyobadilika na yenye hisia kali kisiasa hasa kutokana na sera ya Angela Merkel ya kuwakaribisha wahamiaji milioni moja nchini humo mwaka jana.”
Utafiti huo unasema ni raia 54% Ujerumani waliofurahishwa na hatua ya Wasyria kuruhusiwa kuingia nchi yao.
Nchini Uingereza, ambapo serikali imeweka vipimo kwenye idadi ya wakimbizi kutoka Syria wanaoingia humo, idadi hiyo ilikuwa juu katika 72%.
Wajerumani wengi pia hawakuegemea upande wowote walipoulizwa masuala kuhusu uhamiaji na jamii.
Kuhusu suala la watu wa asili na makabila mbalimbali kuoana kwa mfano, 46% ya Wajerumani hawakuwa na msimamo imara. Wengi kati yao hawakujua wajibu vipi na wengine walijibu kisha wakajaribu kufafanua majibu yao wakisema inategemea hali
Hali ni tofauti kabisa nchi nyingine za Ulaya, mfano Ufaransa ambapo watu wengi waliunga mkono ndoa kati ya watu wa asili na dini tofauti.
Barani Ulaya, ni Urusi iliyokuwa na viwango vya juu vya watu waliopinga ndoa za watu wa asili na dini mbalimbali, 43% ya Warusi walipinga vikali ndoa baina ya watu wa asili na makabila tofauti.
Nchini Uhispania, ni 5% pekee waliopinga.
Urusi pia inaonekana kuwa na idadi kubwa ya wanaopinga kuingia kwa wahamiaji nchini mwao. Ni 11% pekee ya Warusi waliohojiwa waliosema wanaweza kufurahia wahamiaji kutoka Syria, kwa mfano, wakiingia nchini mwao.
NdoaTakwimu kutoka kwa utafiti huo zinaashiria pia kwamba kuna tofauti kubwa miongoni mwa wakazi wa Amerika Kaskazini kuhusu wahamiaji. Nchini Canada, 77% ya waliohojiwa walisema wanaunga mkono wahamiaji kuingia nchini mwao. Nchini Marekani ni 55% pekee.
Indonesia ndiyo iliyo na kiwango cha chini zaidi cha utaifa (4%). Badala yake, inaonekana raia wengi wa Indonesia wanajitambulisha na taifa lao.
Dini haitekelezi jukumu muhimu katika jinsi watu wanajitambulisha ikilinganishwa na utaifa.
Nchi pekee inayojitenga nan chi nyingine ni Pakistan, ambapo 43% ya Wapakistani hujitambulisha kwanza kwa dini yao.
Nchini Marekani, 15% wanajitambulisha kwanza kwa dini yao lakini katika nchi nyingi za Ulaya kiwango hicho ni 5% pekee