Recent Posts

PropellerAds

Saturday, April 16, 2016

Wakenya waliofikishwa ICC wafurahia uhuru

Wakenya sita waliokuwa wamefunguliwa mashtaka na
Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita (ICC)
kuhusiana na ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa
2007 wamekusanyika kwa mkutano wa maombi mjini
Nakuru kusherehekea kutamatishwa kwa kesi dhidi ya
Naibu Rais William Ruto na mwanahabari Joshua Sang.
Mji wa Nakuru unapatikana katika uliokuwa mkoa wa
Bonde la Ufa na uliathirika sana wakati wa mapigano
hayo.
Rais Uhuru Kenyatta, aliyekuwa miongoni mwa
waliofunguliwa mashtaka, amekuwa akihimiza maridhiano
na umoja.
Wengine waliokuwa wamefunguliwa mashtaka ni aliyekuwa
mkuu wa polisi Meja Jenerali Hussein Ali, aliyekuwa
mkuu wa utumishi wa umma Francis Muthaura na waziri
wa zamani Henry Kosgey.
Watu takriban 1,300 walifariki na wengine 600,000
wakafurushwa makwao, wengi wao eneo la Bonde la
Ufa, wakati wa mapigano hayo.
Mahakama ya ICC awali ilithibitisha mashtaka dhidi ya
Bw Kenyatta, Bw Ruto na Bw Sang lakini kesi dhidi
ya Bw Kenyatta ikaondolewa Desemba mwaka 2014.
Kesi dhidi ya Bw Ruto na Bw Sang ilitamatishwa na
majaji mapema mwezi huu.
Mwendesha mashtaka mkuu wa mahakama ya ICC Fatou
Bensouda alikuwa amelalamika kwamba mashahidi wengi
wamehongwa au kutishwa na wakabadilisha ushahidi
waliokuwa wametoa awali na wengine wakajiondoa.
Ruto: Waathiriwa wa ghasia lazima wapate haki
Bensouda: Kenya haikushirikiana na ICC
Ruto ashinda rufaa mahakama ya ICC
Wakati wa kutamatisha kesi dhidi ya Bw Ruto na Bw
Sang tarehe 5 Aprili, Jaji Chile Eboe-Osuji kwenye
uamuzi wake alisema huenda kuingiliwa kwa mashahidi
kulidhoofisha kesi hiyo.
Aidha, alisema kulikuwa na uingiliaji wa kisiasa ambao
huenda uliwatia hofu baadhi ya mashahidi.
Wiki hii, mjadala kuhusu kesi hizo umefufuliwa tena
baada ya kiongozi wa upinzani Raila Odinga kukosoa
hatua ya ICC kutamatisha kesi dhidi ya viongozi wakuu
Kenya.
Alisema hilo huenda likawafanya viongozi na wanasiasa
Afrika kutozingatia mfumo wa sheria wanapotawala.
Bw Odinga alidai kwenye mahojiano na shirika la
habari la AFP kwamba kutokana na uamuzi huo wa
ICC, viongozi wengi wa kiafrika watakuwa madikteta na
hawataogopa kushtakiwa na ICC kwa vile wanaweza
kuhitilafiana na ushahidi bila kujali madhara yake.
Bw Kenyatta na Bw Ruto wakijibu madai hayo kwenye
mkutano wa hadhara eneo la Nyandarua, katikati mwa
Kenya, walimshutumu Bw Odinga wakisema alitaka
kujifaidi kisiasa kupitia kesi hizo.
Hisia miongoni mwa Wakenya zimegawanyika baadhi
wakisema kuna haki ya kusherehekea kutamatishwa kwa
kesi dhidi ya Wakenya hao.
Kuna wengine hata hivyo wanaoamini kwamba si haki
kusherehekea ikizingatiwa kwamba wengi wa waathiriwa
wa ghasia hizo bado wanateseka.
Kwenye Twitter, mgawanyiko huo unajitokeza wazi
kukiwa na vitambulisha mada vinavyoshindana.
Wanaounga mkono mkutano huo wa Afraha, Nakuru na
kuhimiza maridhiano wanatumia kitambulisha mada
#WeAreOneAfraha (Sisi tuna umoja Afraha) na
#UhuruRutoThanksgiving (Ibada ya kutoa shukrani ya
Uhuru na Ruto).
Wanaotetea waathiriwa, kuna kitambulisha mada cha
#WhatAboutTheVictims (Na Waathiria hatima yao
gani).