Recent Posts

PropellerAds

Wednesday, May 25, 2016

Hukumu kesi ya shambulio la Al-Shabab Uganda

Mahakama mjini Kampala leo inatarajiwa kutoa
hukumu katika kesi ambapo wanaume 13
wameshtakiwa kuhusiana na mashambulio ya mabomu
yaliyotekelezwa na al-Shabaab mwaka 2010.
Watu zaidi ya 70 walifariki kwenye mashambulio hayo
yaliyotekelezwa watu wakitazama fainali ya Kombe la
Dunia la mwaka 2010.
Kesi hiyo imechukua miaka sita.
Baadhi ya washtakiwa walikuwa wameambia
mahakama kwamba waliteswa na maafisa wa ujasusi
wa kanda, Marekani na Uingereza.
Lakini mahakama ya kikatiba nchini Uganda ilifutilia
mbali madai hayo.
Washtakiwa 13
Washukiwa ni 13 kutoka Uganda, Kenya na Tanzania.
Saba ni Waganda, 5 Waenya na mmoja anatoka
Tanzania.
Wao ni: Bw Habib Suleiman Njoroge, Isa Ahmed Luyima
Abubaker Betamatory na Dkt Ismail Kalule.
Wengine ni Suleiman Hijar Nyamandondo, Hassan
Haruna Luyima, Hussein Hassan Agade, Bw Idris
Magondu, Mohamed hamid Suleiman na Yahya
Suleiman Mbuthia.
Kutokea kwa shambulio
Shambulio lilifanyika 11 Julai, 2010 na vituo viwili
vilishambuliwa Ethiopian Village Restaurant, Kabalagala
na Kyadondo Rugby Club, Nakawa watu waliopokuwa
wamekusanyika kutazama fainali ya Kombe la Dunia
iliyokuwa ikichezewa Afrika Kusini.
Idadi ya wahanga
Watu 74 walifariki katika shambulio hilo na wengine 70
kujeruhiwa. Takriban watu 60 waliouawa ni wa kutoka
Uganda. Wengine waliofariki dunia ni kutoka mataifa ya
Ethiopia, Eritrea, India na Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Kongo pamoja na mmoja kutoka Ireland na Marekani.
Kuendeshwa kwa kesi
Kesi ilianza miaka mitano baadaye baada ya
kucheleweshwa na hatua ya washukiwa kupinga
kupelekwa kwao nchini Uganda na kudai kuteswa na
vikosi vya usalama.
Lakini Oktoba 2014 mahakama ya kikatiba ilitupilia
mbali kesi yao na hivyo kesi kuanza.
Wanashtakiwa makosa ya: ugaidi, mauaji na kuwa
wanachama wa kundi la kigaidi.
Jaji wa mahakama kuu aliyesikiliza kesi hiyo ni jaji
Alfonso Owiny Dollo.
Mwendesha mashtaka kuuawa
Wakati mmoja muongoza mashtaka aliuawa na watu
wasiojulikana waliokuwa na bunduki.