Recent Posts

PropellerAds

Thursday, May 19, 2016

Hollande: Ndege ya Misri ilianguka

Charles
Rais wa Ufaransa Francois Hollande amesema habari zilizopatikana kufikia sasa zinaashiria ndege ya shirika la ndege la EgyptAir iliyotoweka ikiwa safarini kutoka Paris kwenda Cairo ilianguka.
Hata hivyo amesema bado ni mapema kusema kwa ufasaha kabisa nini kiliisibu ndege hiyo safari nambari MS804, na kwamba bado kuna uwezekano kwamba ilitoweka kutokana na sababu nyingine.
"Taarifa tulizokusanya kufikia sasa, mawaziri, maafisa wa serikali na, bila shaka, maafisa wa Misri, zinathibitisha, kwa huzuni, kwamba ndege ilianguka. Ilitokomea.”
Bw Hollande ameahidi kwamba serikali yake itatoa usaidizi unaohitajika na maafisa wa Ugiriki na Misri wanaoendelea na juhudi za kuisaka ndege hiyo.
 
Ofisi ya mwendesha mashtaka wa Paris nayo imesema imeanzisha uchunguzi kuhusu kutoweka kwa ndege hiyo iliyokuwa imepaa kutoka uwanja wa ndege wa Charles de Gaulle, Paris ikiwa na raia 15 wa Ufaransa.
Ndege hiyo pia ilikuwa na raia 30 wa Misri, raia 2 wa Iraq na raia mmoja mmoja kutoka Uingereza, Canada, Ubelgiji, Kuwait, Saudi Arabia, Algeria, Sudan, Chad na Ureno.
Waziri Mkuu wa Misri Sherif Ismail ameambia wanahabari kwamba juhudi za kuitafuta ndege hiyo bado zinaendelea.
Maafisa wa Misri na Ugiriki wanatumia ndege na meli kuitafuta ndege hiyo katika bahari ya Mediterranean.
Ndege hiyo ilikuwa imewabeba watu 66 ilipotoweka kilomita 16 ndani ya anga ya Misri.