Recent Posts

PropellerAds

Friday, May 13, 2016

Papa aruhusu mjadala wa wanawake mashemasi

Papa aliahidi kubuni tume kutafiti na kujadili uwezekano huo wa kuwezesha wanawake kuhudumu katika ngazi hiyo ambayo ni daraja moja tu chini ya makasisi. Wanahistoria wanasema zamani wanawake walihudumu kama mashemasi.
Papa Francis akiwa Vatican.
Mkuu wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis, amesema ataunda tume itakayochunguza na kujadili uwezekano wa wanawake kuteuliwa kuwa mashemasi katika Kanisa hilo katika pendekezo linaloashiria uwazi wa kuruhusu wanawake kuteuliwa kuhudumu katika nafasi ambazo zimekuwa za wanaume pekee. Wazo hilo tayari limeanza kuibua hisia mbalimbali.
Ni katika mkutano wake maalum na waumini wanawake 900 waliojumuika Vatican ambapo katika awamu ya maswali, suala hilo likaibuka. Papa aliulizwa ikiwa atakuwa radhi kuruhusu utafiti kufanywa kuhusu uwezekano wa wanawake kuwa mashemasi, jambo ambalo ni kinyume na kanuni za sheria za kanisa hilo. Papa aliahidi kubuni tume kutafiti na kujadili uwezekano huo wa kuwezesha wanawake kuhudumu katika ngazi hiyo ambayo ni daraja moja tu chini ya makasisi. Wanahistoria wanasema zamani wanawake walihudumu kama mashemasi.
Robert Gahl ambaye pia ni kasisi na pia profesa wa maadili katika chuo kikuu cha kikatoliki Pontifical University of the Holy Cross anasema "Kile ambacho Papa anatafakari ni uchunguzi wa kihistoria kuhusu majukumu ambayo mashemasi wanawake walikuwa wakifanya, na kufikiria kuyazingatia ili kuwezesha wanawake katika njia moja ya ushemasi. Hata hivyo tutarajie kuwa papa hatahimiza kitu kama hicho kwa sababu tayari ameshasema hataki wanawake kuwa makasisi. Analotaka ni kuwezesha wanawake katika jamii".
Wanawake kanisani maarufu Sisters.
Kauli ya Papa ilipokelewa vema na baraza la kutawaza wanawake WOC, shirika la Marekani linalohimiza kanisa katoliki kuanza kutea na kutawaza wanawake katika ngazi zote za huduma kanisani ikiwemo ukasisi. Papa Francis ameonekana mara kwa mara akihimiza usawa wa kijinsia. Kate Mc Elwee ambaye ni mkurugenzi wa baraza la uteuzi wa wanawake, ni kati ya wale ambao wamesifia kauli ya Papa kwa kukubali mjadala huo ufanywe. Amesema "Ninafikiria kuwa Papa kweli anataka swali hilo lijadiliwe. Maandiko yetu wenyewe na wahubiri wametuambia kuwa wanawake sawa na wanaume wamekuwa mashemasi tangu zamani, kwa hivyo ninafikiria tume itaunga mkono historian a itakuwa bora ikiwa Vatican itakubaliana na hilo"
Mashemasi hutawazwa kuwa wahudumu tu wa kanisa lakini si makasisi. Japo wanaweza kutekeleza majukumu mengineyo yanayofanywa na makasisi, kama vile kuongoza sherehe za harusi, ubatizo na hata kuhubiri, hawawezi kuongoza misa ya Pasaka.
Kadhalika amerudia mara kwa mara kuwa hataki kuwakilisha mafunzo yote ya kanisa kana kwamba yameandikwa kwenye jiwe. Amejaribu kufanya kanisa kuwa na uelawa na kutofanya maamuzi dhidi ya waliotalikiana, wanaowekeana kimada na waumini ambao ni wapenzi wa jinsia moja